OR NA MBLM ZANZIBAR YAFANYA KIKAO NA IDARA YA UHAMIAJI ZANZIBAR

  • Nov 30, 2017
  • 157 Views

Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa kimataifa na Uratibu wa Wazanzibari wanaoishi nchi za nje Adila Hilal Vuai amesema kuwa Idara yake inakusudia kujenga mashirikiano ya karibu zaidi na Idara ya Uhamiaji Zanzibar ili kuona inazipatia ufumbuzi wa haraka baadhi ya changamoto wanazozipata wanadiaspora wakati wanapoingia au kutoka nchini.

Akizungumza katika kikao cha kwanza cha pamoja kati ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Idara ya Uhamiaji Zanzibar na wakilishi wa wanadiaspora kutoka sehemu tofauti duniani kilichofanyika Ikulu, Mkurugenzi Adila amesema miongoni mwa njia nzuri ambazo zinaandaliwa kwa pamoja kati ya Idara yake na Idara ya Uhamiaji ni kuziangalia changamoto wanazokuwa wanazipata Wanadiaspora kwa kuzijadili na kupendekeza njia sahihi zitakazopelekea kutatua changamoto hizo hasa zile za kiuhamiaji.

Nae Naibu Kamishna wa Idara ya Uhamiaji Zanzibar Abdul Mabrouk Kitwana amewasisitiza Wanadiaspora kabla ya kufanya uamuzi wa kuchukua uraia wa kigeni wanapaswa kuzisoma vizuri sheria na kanuni za uhamiaji za Tanzania namna zinavyoelekeza na kuzifahamu ipasavyo ili kuepukana na changamoto zinazoweza kuepukika, kwa kuwa utekelezaji wa sheria za uhamiaji hauwezi kwa sasa kutoa upendeleo kwa kuwatofautisha wanadiaspora na wegeni wengine.

Alisema kwamba inawezekana kuwa Mwanadispora ni Mzanzibari halisi lakini inapokuwa unabadilisha uraia na kuwa na pospoti ya nchi nyengine hadhi yake ya ukaazi inakuwa imebadilika hivyo mtu huyo anapaswa kufuata sheria na taratibu zilizowekwa na wala sio kwa lengo la kukomolewa kama badhi yao wanavyofikiria bali ni kwa kutekeleza sheria na taratibu za nchi ( tanzania).

Picha No. 03.v011

Related Articles